Hebrews 2

Wokovu Mkuu

1 aKwa hiyo, imetupasa kuwa waangalifu sana kuhusu kile tulichosikia, ili tusije tukakiacha. 2 bKwa kuwa kama ujumbe ulionenwa na malaika ulikuwa imara, na kila uasi na kutokutii kulipata adhabu ya haki, 3 cje, sisi tutapaje kupona kama tusipojali wokovu mkuu namna hii? Wokovu huu, ambao mwanzo ulitangazwa na Bwana, ulithibitishwa kwetu na wale waliomsikia. 4 dPia Mungu aliushuhudia kwa ishara, maajabu na kwa miujiza mbalimbali, na karama za Roho Mtakatifu alizozigawa kulingana na mapenzi yake.

Isa Alifananishwa Na Ndugu Zake

5 eMungu hakuuweka ulimwengu ujao ambao tunanena habari zake chini ya malaika. 6 fLakini kuna mahali mtu fulani ameshuhudia akisema: “Mwanadamu ni kitu gani hata unamfikiria,
binadamu ni nani hata unamjali?

7 Umemfanya chini kidogo kuliko malaika;
ukamvika taji ya utukufu na heshima,

8 gnawe umeweka vitu vyote chini ya miguu yake.”

Kwa kuweka vitu vyote chini yake, Mungu hakuacha kitu chochote ambacho hakukiweka chini ya mwanadamu. Lakini kwa sasa, hatuoni kwamba kila kitu kiko chini yake.
9 hLakini twamwona Isa, aliyefanywa chini kidogo kuliko malaika, sasa akiwa amevikwa taji ya utukufu na heshima kwa sababu alistahimili mauti, ili kwamba kwa neema ya Mungu apate kuonja mauti kwa ajili ya kila mtu.

10 iIli kuwaleta wana wengi katika utukufu, ilifaa kwamba Mungu, ambaye ni kwa ajili yake na kupitia kwake kila kitu kimekuwepo, amkamilishe mwanzilishi wa wokovu wao kwa njia ya mateso. 11 jYeye awafanyaye watu kuwa watakatifu, pamoja na hao ambao hufanywa watakatifu, wote hutoka katika jamaa moja. Hivyo Isa haoni aibu kuwaita ndugu zake. 12 kYeye husema, “Nitalitangaza jina lako kwa ndugu zangu;
mbele ya kusanyiko nitaimba sifa zako.”

13 lTena, “Nitaweka tumaini langu kwake.”

Tena anasema, “Niko hapa, pamoja na watoto ambao Mungu amenipa.”

14 mBasi kwa kuwa watoto wana nyama na damu, yeye pia alishiriki katika ubinadamu wao, ili kwa kifo chake, apate kumwangamiza huyo mwenye nguvu za mauti, yaani ibilisi, 15 nna kuwaweka huru wale waliokuwa utumwani maisha yao yote kwa sababu ya kuogopa mauti. 16 oKwa kuwa ni dhahiri kwamba hakuja kusaidia malaika, bali uzao wa Ibrahimu. 17 pKwa sababu hii ilibidi afanane na ndugu zake kwa kila hali, ili apate kuwa Kuhani Mkuu mwenye huruma na mwaminifu katika kumtumikia Mungu, ili pia apate kufanya upatanisho kwa ajili ya dhambi za watu. 18 qKwa kuwa yeye mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wale wanaojaribiwa.
Copyright information for SwhKC